AnuaniKisiwandui, Zanzibar
Simu(+255) 26 23 22965

Habari na Matukio Mbalimbali


SERIKALI ITAONGEZA NGUVU KUUENZI MJI MKONGWE

alternative

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema itaongeza nguvu ya pesa kuuenzi na kuudhibiti Mji Mkongwe uendelee kuwa na haiba nzuri ya urithi wa kimataifa.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo kwenye ufunguzi wa Hoteli ya Tembo awamu ya pili, iliyopo Mji Mkongwe, wilaya ya Mjini mkoa wa mjini Magharibi inayomilikiwa na mfanyabiashara, Hussein Sadik Muzzamill na familia yake.

Alisema, fedha hizo zitatengeneza mifumo mipya ya maji, kuweka sawa nyaya za umeme na kuboresha barabara zote za mji huo kwa kiwango cha lami na vigae, ikiwemo maegesho ya magari ili kuongeza ubora na uimara utakaovutia watalii wengi.

Dk. Mwinyi alisema ufunguzi wa jengo la Hoteli mpya ya Tembo ni miongoni mwa jitihada za Serikali kuwadhihirishia wananchi wake jinsi ilivyojipanga kuyaenzi na kuyadumisha majengo hayo yaendelee kuishi kwa zaidi ya miaka 200 na kuongeza matengenezo na ukatarabati wa yumba kongwe ni dhamira yake kuendelea kuuenzi na kuutunza Mji Mkongwe ubakie kwenye hadhi yake ya asili.

Alisema, Mji Mkongwe unaitofautisha Zanzibar na nchi nyengine za Visiwa duniani kwani wao wanafukwe na Zanzibar ina fukwe na Mji Mkongwe.

Alieleza Serikali inatarajia usimamizi wa usafi wa mji huo, kurejeshwa kwenye mamlaka ya Mji Mkongwe ili waendelee kuusimamia na kuboresha mandhari na haiba ya mji huo ulingane na hadhi ya kimataifa kwa kuwa kivutio bora kwa watalii.

“Nataka nikimaliza muda wangu wa uongozi Mji Mkongwe urudi kuwa kama zamani kwa mvuto wa haiba yake ya mandhari yenye kumpendezesha kila anaeutembelea” aliahidi Dk. Mwinyi.

Vile vile Dk. Mwinyi aliishukuru Serikali ya Oman kwa msaada wao wa kukarabati jengo la Beit el Ajaab wa dola za Marekani milioni 21 na kuongeza kwamba Serikali inadhamira ya kuendelea kukarabati majengo mengine ya Mji Mkongwe ili kuyarejeshea hadhi yake likiwemo jengo la “People’s Palace”

Katika hatua nyengine, Rais Dk Mwinyi aliwapa miezi mitatu waliopewa nyumba za Serikali kuzikatabati nyumba hizo, lengo ni kuwapa watu wazitunze ili ziendelee kudumu zaidi.

Dk. Mwinyi pia aliitaka Mamlaka ya Mji Mkongwe kuboresha maeneo yote ya wazi kuwa vivutio kwa watalii na wageni wanaoutembelea mji mkongwe pamoja na kujenga bustani nzuri zenye hadhi ya kimataifa na kuahidi kuikarabati upya bustani ya Forodhani. 

Rais Mwinyi pia aliiagiza Mamlaka ya Mji Mkongwe kupanga utaratibu mzuri kwa wafanyabiashara wa eneo hilo ili kuweka mandhari yenye mvuto kwa wageni wanaoutembelea mji huo na kuendelea kuwa sehemu salama kwao na wenyeji wanaotembelea hapo.

Aliongeza lengo la ukarabati wa mji huo ni kuhifadhi uwe na hadhi ya kimataifa kulingana na mataifa mengine duniani yenye urithi wa kimataifa. 

“Nataka bustani ya Forodhani irejeshwe kwenye hadhi ya kimataifa, mara hii tutatumia nguvu zetu kuiboresha, kujengwe sehemu za watu kupumzikia na kuhakikisha jamii inazitunza bustani za Mji Mkongwe” alieleza Dk. Mwinyi

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Simai Mohamed Said alisema familia ya Muzzamill imetoa mchango mkubwa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kukarabati Dau Palace, jengo la Mizingani na kutoa mchango mkubwa kuikarabati bustani ya Forodhani. 

Pia Waziri Simai alieleza Tembo hotel imeendelea kuisaidia Serikali kwa kutoa ajira nyingi kwa wazawa, vijana wa Zanzibar, aidha aliongeza kwamba Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale inafanyakazi kwa ushirikiano mkubwa na taasisi zake katika kuufanya Utalii wa Zanzibar kuendelea kuimarika kwa kutekeleza maono ya Serikali ya awamu ya nane ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kufanikisha adhma ya kuifikisha mbali Zanzibar kimaendeleo kupitia sekta ya Utalii.

Naye, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Mji mkongwe Zanzibar, Ali Said Bakar alisema ukarabati wa jengo la Tembo Hotel ulizingatia vigezo vyote vya kimataifa vilivyowekwa na UNESCO kwa kubakisha thamani za asili, pia alimuahidi Rais kuendelea kuweka mji mkongwe kuwa safi kwa kutekeleza agizo lake la kuweka sawa nyaya zote ya umeme, simu na ving’wamuzi zilizotapakaa kwenye mji huo kuwa na mwonekano sahihi.

Kwa upande wake Mmiliki wa hoteli ya Tembo, Hussein Sadik Muzzamill alisifu juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanibar za kuendelea kuwaletea maendeleo Wazanzibari wote na kuahidi kuendelea kuunga mkono juhudi hizo.

Jengo jipya la hoteli ya tembo asili yake lilikua ubalozi wa Marekani mwaka 1831, kisha likaendelea kutumiwa kwa shughuli za Serikali, mwaka 1944 lilikuwa skuli na pia liliwahi kuwa Wizara ya Ardhi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Habari Nyingine
Albamu