AnuaniKisiwandui, Zanzibar
Simu(+255) 26 23 22965

Habari na Matukio Mbalimbali


CCM ZANZIBAR YAIPONGEZA ZIPA

alternative

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimesema kimeridhishwa na utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM katika eneo la uwekezaji kupitia Mamlaka ya Vitega Uchumi Zanzibar(ZIPA).

Kauli hiyo ameitoa jana Katibu wa Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Khamis Mbeto Khamis mara baada ya kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji ZIPA,Shariff Ali Shariff ofisini kwake Maruhubi.

Alisema ZIPA imetekeleza kwa kiasi kikubwa azma ya Rais wa wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi ya kuwavutia wawekezaji ambapo miradi mingi tayari imekwishawekezwa kwa kipindi kifupi.

"Eneo la uwekezaji ndio uti wa mgongo wa uchumi wa Zanzibar hivyo niwapongeze ZIPA kwa kazi nzuri mnayoifanya na kasi kubwa mnayoitekeleza ya ilani ya chama chetu," alisema.

Katibu huyo aliitaka ZIPA kuendelea kufanya kazi kwa  karibu na CCM ili kufikia malengo ya ilani ya uchaguzi katika kuwaletea maendeleo wazanzibari.

Naye, Mkurugenzi wa ZIPA Sharif Ali Sharif, alisema, mwekezaji anapotaka kuwekeza anapewa masharti kwa kuhakikisha anazingatia mazingira ya uwekezaji yenyewe.

Alisema kwa sasa ZIPA imekuwa na uwekezaji wa miradi mikubwa 226 ambayo inaweza kuzalisha dola za kimarekani bilioni 3.5 ambapo inatengeneza ajira zaidi ya 13000.

"Katika kipindi cha miaka hii miwili ya serikali ya awamu ya nane ZIPA kupitia serikali tumetekeleza ilani kwa vitendo jambo ambalo imeonyesha dhamira kwa serikali kuhakikisha uchumi unaongezeka,"alisema

Alisema katika kipindi cha miaka miwili wawekezaji wameongezeka kutokana na kupata ushirikiano mkubwa kutoka kwa Rais, Dk. Mwinyi kutokana na kuwa ametengeneza mazingira mazuri kwa wawekezaji.

"Rais Dk.Mwinyi ameiimarisha ZIPA kiutendaji kwani Mamlaka hii imekuwa na watendaji wenye uwezo mkubwa wa kitaalamu katika kuwavutia wawekezaji na pia wameweka sheria ambayo ni rafiki zaidi kwa wawekezaji,"alisema

Alisema kupitia miradi hiyo zimepatikana ajira mbalimbali kwa wananchi wa Zanzibar na kwamba lengo la serikali ni kuhakikisha uchumi wa unaongezeka kwa asilimia kubwa.

Pia, alisema uwekezaji umeongezeka kutokana na serikali kuanzisha kituo cha pamoja ambacho kinatoa huduma zote kwa wakati mmoja ambapo wawekezaji wamekuwa wakirahisisha upatikanaji wa huduma hizo kwa wakati.

Akizungumzia upande wa visiwa, Mkurugenzi Sharif, alisema, kibali kinachotolewa kwa muwekezaji hupewa masharti ya asilimia 10 ya eneo husika na asilimia iliyobakia hupewa masharti ya kujenga ndani ya eneo la baharini ili kuona visiwa hivyo havihathiriki na uwekezaji huo.

Mkurugenzi huyo alisema katika uwekezaji huo,muwekezaji utanguliza fedha kabla ya kuwekeza ambapo kwa sasa serikali imeshaingiza dola za kimarekani milioni 14 ambapo katika miradi ya visiwa hivyo inatakiwa kuingiza dola za kimarekani milioni 19.

"Wawekezaji hawa wamekuwa wakilipa kwa awamu na fedha zilizoingia zipo na zitatumika kwa matumizi mbalimbali ikiwemo kulipwa fidia watu waliokuwepo katika bahari ikiwemo wavuvi, na wawekezaji ambao hawakufikia vigezo tunavyovitaka," alisema

Akizungumzia suala la viwanda ndani ya visiwa vidogo alisema, katika uwekezaji huo kutotakiwa uwekezaji wa  viwanda vikubwa na kwamba viwanda vinavyotakiwa ni vya kati na vyepesi ambavyo vitakuwa na thamani kubwa.

Mbali na hilo,alisema ZIPA itaendelea kutekeleza ilani ya CCM katika utendaji wao wa kazi wa kila siku na kufuata miongozo ya Rais Dk.Mwinyi juu ya uwekezaji nchini.

Habari Nyingine
Albamu